

NA MWANDISHI WETU, TANDAHIMBA
Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe ametoa mifuko 200 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa Msikiti wa Wilaya ya Tandahimba mkoani Mtwara.
Msaada huo ni ahadi yake aliyoitoa mwaka jana 2022 alipokuwa kwenye ziara ya kuimarisha chama chake mikoa ya Kusini.
Msaada huo umekabidhiwa leo Mei 26, 2023 na Mjumbe wa Kamati Kuu wa ACT Wazalendo, Isihaka Mchinjita kwa niaba ya Zitto.
Akikabidhi msaada huo, Mchinjita ambaye ni Mwenyekiti wa Wilaya ya Lindi na mlezi wa Mkoa wa Mtwara wa chama hicho alimshukuru Mungu kwa kuwezesha ahadi hiyo kutimizwa huku akiwakumbusha wadau wengine kusaidia ujenzi wa msikiti huo ili ukamilike kwa wakati.
“Kwa niaba ya Kiongozi wa chama, Ndugu Zitto Kabwe napenda kukabidhi msaada huu wa mifuko 200 ya saruji baada ya kuombwa na uongozi wa Msikiti huu kupitia risala yenu mwaka jana 2022.
“Akiwa kwenye ziara ya ujenzi wa chama mwaka jana 2022 mlimwomba Kiongozi wa chama kusaidia chochote alichonacho ili kuwezesha ujenzi huu, hivyo ahadi yake kwenu amenituma nije kuikabidhi leo.”alisema Mchinjita.
Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Imamu wa Msikiti Mkuu wa Ijumaa ambao ni wa Wilaya ya Tandahimba, Salum Ibun Mwanya alimshukuru Zitto kwa kutimiza ahadi yake hiyo huku akiomba wadau wengine kuguswa na ujenzi huo wa nyumba ya kuabudia.