WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezindua jengo la wagonjwa wa dharura kwenye hospitali ya wilaya ya Ruangwa ambalo limegharimu sh. milioni 390.
Akizungumza na wakazi wa Ruangwa waliofika kushuhudia uzinduzi huo leo (Ijumaa, Machi 31, 2023), Waziri Mkuu amesema ameridhishwa na ujenzi huo na hasa kwa vile amekuta kuna vifaa vya kisasa.
“Yote haya ni matunda ya kazi nzuri inayofanywa na Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na yamesaidia kuifanya wilaya yetu iwe miongoni mwa wilaya zinazoenda kwa kasi,” amesema.
Waziri Mkuu amesema hospitali hiyo imejengwa kwenye eneo lenye ukubwa wa ekari 100 ambalo kazi ya kujenga uzio ni kubwa kwa hiyo akawataka wakazi hao wawe walinzi wa miundombinu na vifaa tiba vilivyonunuliwa ili waendelee kupata huduma bora na za uhakika.
“Eneo hili lina ekari 100. Ninaomba sana sisi tuwe walinzi wa vifaa hivi vilivyopo hapa ndani na kamwe tusishiriki mpango wowote wa kurudisha maendeleoa nyuma,” amesisitiza.