Kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa Bw. Abdallah Shaib Kaim, amewaasa wananchi kuacha kufanya shughuli za kibinadamu karibu na maeneo ya vyanzo vya maji ili kunusuru upotevu wa maji.
Wakati wa zoezi la upandaji miti katika bwawa la Mindu mkoani Morogoro kiongozi huyo wa mbio za mwenge amesema serikali inaendelea na mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwa kuhifadhi mazingira na kutunza vyanzo vya maji.
Pia kiongozi huyo wa mbio za mwenge ameipongeza Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu kwa kutii agizo la serikali lililotolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango,likielekeza Bodi zote za maji kupanda miti zaidi ya milioni mbili.
Bwawa la Mindu ni miongoni mwa vyanzo vya maji 231 vinavyosimamiwa na Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu mkoani Morogoro, bwawa hilo linategemewa kwa asilimia 75 ya wakazi wa Manispaa ya Morogoro.