Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, imesema kuna baadhi ya wamiliki wa makao ya watoto wamekuwa na tabia ya kuendesha vituo hivyo kwa maslahi yao binafisi jambo ambalo ni kinyume cha sheria na kwamba kwa watu ambao watabainika kuwatumia watoto kwa masilahi yao binafisi hatua kali zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kufutiwa usajili.
Hayo yamebainishwa na Naibu waziri wa maendeleo ya jamii,jinsia wanawake na makundi maalum,Mwanaid Ali Khamis wakati akizungumza kwenye kituo cha watoto cha Moyo wa Huruma kilichopo Mjini Geita.
Amesema kuna baadhi ya wamiliki wa vituo vya kulelea watoto, wamekuwa wakiwapiga picha na kuchukua video na kusambaza matangazo kwenye mitandao kwa nia ya kujipatia fedha kutoka kwa wahisani jambo ambalo ni kosa kwa mujibu wa sheria ya watoto.
“Baadhi ya wamiliki wamekuwa na tabia ya kuwapiga picha watoto na video kisha kusambaza matangazo kwenye mitandao kwa lengo la kujipatia fedha kutoka kwa wahisani jambo hili ni kosa kwa mujibu wa sheria ya mtoto ya mwaka 2009 na siku hizi kuna wafadhili hawaamini hususani wa huko nje kwani wamekuwa wakitoa msaada kwa kuwafundisha mambo ambayo ni kinyume na tamaduni za kitanzania hivyo niwaombe wenye tabia za namna hii waache mara moja” Mwanaid Ali Khamis, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.