Na JOSEA SINKALA
Serikali imesema vijiji vyote ambavyo vipo kwenye Mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili vitakamilika ifikapo Disemba 2023.
Hayo yameelezwa Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Steven Byabato wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini Mhe. Oran Njeza alipouliza ‘Je, ni lini Serikali itapelekea umeme kwenye vijiji vya Kata ya Shizuvi ambavyo ni sehemu ya REA awamu ya 3 mzunguko wa pili?’
Akijibu swali hilo Naibu Waziri Byabato amewatoa hofu wananchi kwamba vijiji ambavyo vimekwisha orodheshwa kwenye REA awamu ya tatu kufikia mwishoni mwa mwaka huu vitafikiwa na nishati hiyo.
“Vijiji vyote ambavyo vipo kwenye mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili vitakamilika ifikapo Disemba mwaka huu 2023. Nimuhakikishie Mheshimiwa Oran Njeza kwamba vijiji hivyo pia katika kata hizo (Shizuvi) vitakuwa vimefikiwa na umeme kabla ya Disemba mwaka huu,” Ameeleza Naibu wa Nishati Steven Byabato, kwenye mkutano wa Bunge unaoendelea jijini Dodoma.
Mara kwa mara Mbunge wa Mbeya Vijijini na Mwneyekiti wa wabunge wa mkoa wa Mbeya na mjumbe wa Kamati ya bajeti na fedha Mhe. Oran Njeza amekuwa akiikumbusha Serikali kuhakikisha inafikisha umeme kwa wananchi wake huku akiwahimiza wananchi kupitia viongozi wao wa vitongoji na vijiji kuendelea kusuka miundombinu ya umeme na kuorodhesha majina yao kwa wakala wa usambazaji umeme vijijini REA ili mpango huo unapokamilika kwa awamu wafikiwe na nishati hiyo muhimu hasa katika ujenzi wa Serikali ya Viwanda.