Wakazi wa kata ya Iganjo Jijini Mbeya wameomba Serikali kutatua kero zao za Miundombinu ya barabara maji, umeme na upatikanaji wa huduma za afya kwa wazee katika hospitali ya wilaya ya Igawilo Jijini Mbeya.
Wakieleza kero hizo kwenye Mkutano wa hadhara wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Comrade Beno Malisa, Wananchi hao wamesema Serikali ishughulikie na kutatua kero za maji na umeme, Miundombinu ya Barabara ikiwemo kuweka alama za barabarani ili kupunguza ajali lakini pia kuboresha huduma za Afya katika hospitali ya Wilaya Igawilo ikiwemo upatikanaji wa dawa na kuongeza Watumishi bila kusahau kupewa kipaombele wazee katika huduma.
Mkuu wa Wilaya ya Mbeya akiongozana na Wataalam mbalimbali wametolea ufafanuzi wa malalamiko hayo ikiwemo uboreshaji huduma za afya kuboresha Miundombinu ya Maji na kusambaza maji maeneo ambayo hayajafikiwa na huduma ya Maji katika kata hiyo.
Ziara ya Mkuu wa Wilaya imekamilika kwa kuwataka wananchi kushirikiana na Serikali katika kuleta maendeleo na kuwahakikishia kuwa Serikali itajitahidi kutatua changamoto hizo.