Baraza kuu la Waislam (BAKWATA) mkoa wa Katavi limefanya dua maalum ya kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kutokana mageuzi makubwa ya kimaendeleo kwenye utawala wake.
Akiwaongoza waumini mbalimbali wa Kiislam mkoani humo, sheikh wa Mkoa wa Katavi Sheikh Mashaka Nasoro Kakulukulu amesema baraza hilo limeamua kumuombea dua hiyo Rais Samia kama shukrani, kwani vitu alivyoufanyia mkoa wa Katavi ni mengi kwa kipindi kifupi na hakuna namna nyingine ya kumlipa.
Aidha amesema hawataishia hapo bali wataendelea kumuombea kila mara ili Mwenyezi Mungu ampe nguvu na utayari wa kuendelea kuwaletea maendeleo watanzania.
Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi Hassan Rugwa ambaye alikuwa mgeni rasmi katika dua hiyo amewapongeza waumini wa Kiislam waliojitokeza kushiriki dua hiyo na kuwaomba kuendelea kumwombea Rais Samia na viongozi wengine kwa Mwenyezi Mungu awaongoze katika njia bora ya kuwaongoza wananchi.
Nao baadhi ya washiriki wa dua hiyo wamepongeza uongozi wa BAKWATA mkoa wa Katavi kwa kufanya dua hiyo wakidai kuwa kitendo hicho hakijawahi kufanyika na wanaamini kitendo hicho kitampa nguvu na imani zaidi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan na kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati katika mkoa wa Katavi.