Na Joel Maduka Geita.
Mkuu wa Mkoa wa Geita Martine Shigela amewataka wadau wa mazingira kutoka ndani na nje ya Mkoa huo kuendelea kutoa elimu ya utunzaji mazingira ikiwemo upandaji wa miti kwa kuwa eneo hilo linakabiliwa na changamoto ya uharibifu wa mazingira unaochochewa na shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu.
Mhe Shigela ametoa wito huo katika zoezi la uzinduzi wa Kampeni ya upandaji wa miti inayokwenda kwa jina la “Pendezesha Tanzania” inayoratibiwa na Benki ya CRDB kwa lengo la kurejesha uoto kwenye maeneo mbalimbali na zoezi hilo limefanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita.
“Mkoa wetu wa Geita unashughuli nyingi za kibinadamu ambazo zimekuwa zikichochea kuharibu mazingira kama uchimbaji wa madini ya dhahabu hivyo zoezi hili la upandaji wa miti linavyofanywa na Benki ya CRDB ni kichocheo cha kurudisha uoto wa asili ndani ya Mkoa wetu”Martine Shigela Mkuu wa Mkoa wa Geita.
Meneja wa CRDB Kanda ya Magharibi Jumanne Wagana amesema Kampeni ya “Pendezesha Tanzania” ni muendelezo wa utekelezaji wa mikakati ya Benki hiyo kusaidia jitihada za serikali katika kutunza nakuboresha mazingira nakwamba katika mkoa wa Geita watapanda zaidi ya miti 800.
“Leo tunapanda miti 200,hapa Hospital ya Rufaa ya Mkoa wa Geita kupitia Taasisi yetu ya CRDB Foundasheni lengo letu ni kutaka kuona tunarudisha hali safi ya Taifa letu la Tanzania”Jumanne Wagana Meneja wa CRDB Kanda ya Magharibi.