Shirika lisilo la kiserikali la Global Peace Foundation Tanzania limetoa mafunzo yaliyowakutanisha vijana 50 katika ukumbi wa Alpha uliopo Manispaa ya Mtwara Mikindani Mkoani Mtwara yenye lengo la kutoa Elimu juu ya kudumisha amani kwa jamii zinazowazunguka.
Akizungumza katika mafunzo hayo Dkt. Richard Mwaifunga, Mratibu wa masuala ya Vijana kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu amesema;
“Lengo kubwa ni kuhakikisha tunawajengea uwezo vijana kuwa mabalozi wa Amani katika jamii. Hii inaenda sambamba na kuhakikisha vijana hao wanapata na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo katika mkoa huu. Ukweli ni kwamba hakuna amani pasipo maendeleo na hakuna maendeleo kama amani haipo. Dhana hizi mbili zinakwenda pamoja”.
“Serikali imeweka mikakati mingi na imefanya jitihada kubwa lakini nasikitika sana vijana wengi sio waadilifu,sio waaminifu,hamjali hamtaki kuzitumia fursa hamzitafuti nimesikitika katika watu 50 humu hamjawahi kukopa mkopo wa mfuko wa maendeleo ya vijana na naomba niseme kwamba serikali haina deni kwaajili ya vijana fursa zipo munapaswa muzitumie.” anasema Dkt. Richard Mwaifunga, Mratibu wa masuala ya Vijana kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu.
Kwa upande wake Irene Ishengoma, Meneja Tathimini na Ufuatiliaji wa shirika hilo naye alitaja kwa undani fursa zinazotolewa na Serikali ambazo mara nyingi vijana hawajazichangamkia ipasavyo.
“Ziko fursa mbalimbali Serikalini kama mikopo kwa mtu mmoja mmoja na nafasi za elimu. Vijana tuamke usingizini” amesema Irene.