Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Elkana Balandya amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri za mkoa huo kuhakikisha wanazingatia kwa umakini na kwa kutumia utaalamu kuhusiana na majukumu yaliyoshirikishwa ya udhibiti ubora wa bidhaa za chakula na vipodozi.
Rai hiyo ameitoa wakati wa zoezi la kusaini mkataba wa ushirikiano baina Shirika la Viwango Tanzania ( TBS ) na TAMISEMI kwa Wakurugenzi wa Halmashauri za Mkoa wa Mwanza ili kurasimisha zoezi la utekelezaji wa Kanuni ya ushirikiano ya mwaka 2021 katika ngazi za Halmashauri kwa kuzingatia Sheria ya Viwango.
“ Majukumu mliyopewa yakawe chachu ya kutumikia umma kwa bidii bila ubaguzi, kuwashauri na kuwasaidia kitaalamu pale itakapohitajika ili bidhaa ziwe na bora na salama na uchumi uendelee kukua”_ Balandya.
Meneja wa TBS Kanda ya Ziwa Happy Brown, amesema wanatarajia baada ya kusaini mkataba baina ya TBS na Halmashauri bidhaa zitaangaliwa kwa ukaribu katika maeneo mbalimbali mkoani humo yanayotoa huduma kwa kukaguliwa na kukidhi matakwa ya Viwango na vigezo kwa watumiaji.
Baadhi ya viongozi wa serikali na ngazi ya Halmashauri wameudhuria hafla hiyo ya utiaji saini wakiwemo, Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri za Jiji,Manispaa na Wilaya za mkoa wa Mwanza,Mstahiki Meya wa Jiji na Manispaa na Wenyeviti wa Halmashauri za Wilaya za mkoa wa Mwanza na watumishi wa TBS Kanda ya Ziwa.