BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (NACTVET) limezitaka Taasisi za vyuo binafsi kuwa na wakaguzi wa mahesabu ya ndani ili kuepuka changamoto mbalimbali katika uendeshaji wa fedha.
Wito huo ulitolewa jana Mkoani Mbeya na Msaidizi wa Mkuu wa kanda ya nyanda za juu kusini wa baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Japhet Simpepo wakati wa uzinduzi wa bodi mpya ya Taasisi ya Sayansi za Afya Mbalizi inayomilikiwa na Kanisa la Uinjilisti Tanzania.
Simpepo alisema taasisi nyingi za vyuo zinazomilikiwa na watu binafsi hazioni umuhimu wa kuwa na wakaguzi wa mahesabu ya ndani kwa sababu akaunti za vyuo zinamilikiwa na wenyewe hali ambayo inasababisha wakuu wa vyuo kutofahamu mapato ya taasisi na kupata changamoto katika uendeshaji wa bajeti zao
“Uwepo wa bodi hizi ni takwa la kisheria kulingana na mwongozo wa Serikali hivyo tunatoa ari kwa wakuu wa Taasisi hizi waziamini mamlaka wanazozipa mandeti kisheria zikiwemo bodi za ushauri, kufanya kazi kwa uhuru kwani zinakosa nguvu hasa kwenye masuala ya fedha kutokana na akaunti za fedha kumilikiwa na wenye vyuo”Alisema Simpepo.
Katibu Mkuu wa Kanisa la Unjilisti Tanzania Mchungaji Jacobo Mwakasole alisema wao kama wamiliki wa Taasisi hiyo wanatekeleza agizo hilo la Serikali kwa kuwa na wakaguzi wa ndani na kuhakikisha taarifa zote za kifedha zinawekwa wazi na kwamba uwepo wa bodi hiyo utawasaidia kuwashauri kwenye mambo mbalimbali yakiwemo masuala ya kifedha.
Mkuu wa Taasisi ya sayansi za Afya Mbalizi, Shukrani Ndumula alisema taasisi hiyo yenye wanafunzi zaidi ya 1000 imefanikiwa kutoa wataalamu wanaoajirika katika taasisi za umma na binafsi, uboreshaji miundombinu ikiwemo ujenzi wa maabara na mabweni na kupelekea wizara ya Afya kuwapa kibali cha kuongeza kozi nyingine ikiwemo ya utabibu meno.
Akizindua bodi mpya ya Taasisi hiyo Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Beno Malisa aliitaka Taasisi hiyo kuwapa kipaumbele wakazi wa eneo hilo kwenye kila huduma wanazotoa huku akiitaka bodi hiyo kuwa na maono makubwa na kutimiza majukumu yake ipasavyo na kuahidi Serikali kuendelea kutoa ushirikiano kwa Taasisi hiyo.