Spika wa Bunge la Tanzania Tulia Ackson ni miongoni wa wabunge waliowasilisha maombi ya kugawa majimbo yao kutokana na ukubwa na wingi wa watu.
Hayo yamebainishwa leo bungeni na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu Ummy Nderiananga wakati akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Viti Maalum Sophia Mwakagenda.
Mjadala katika maswali na majibu kwa wizara hiyo ulianza kuhusu kugawanywa kwa rasilimali kulingana na ukubwa wa eneo ambapo kulitanguliwa maswali kutoka kwa mbunge wa Kilindi Omari Kigua aliyeuliza ni lini Serikali italigawa Jimbo la Kilindi kutokana na jiografia yake na kufuatiwa na Mbunge wa viti maalum Sophia Mwakagenda aliyeuliza ni lini Serikali italigawa jimbo la Mbeya mjini ambalo linaongozwa na Spika wa Bunge Tulia Ackson kutokana na ukubwa wake.
Katika majibu ya Naibu waziri Nderiananga amesema “Mheshimiwa Tulia Ackson alishawasilisha kwenye mamlaka nia ya kuomba jimbo hilo ligawanywe, Serikali inatafakari maombi hayo na wakati utakapofika vigezo vitatazamwa,”
Amesema kwa sasa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ipo katika maandalizi mbalimbali ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 hivyo kwa kuzingatia taratibu na vigezo, muda wa kugawa majimbo utakapofika Tume itatoa tangazo rasmi kwa wadau wote wa uchaguzi juu ya kuanza kwa machakato wa ugawaji wa majimbo.