NA JOSEA SINKALA, MBEYA.
Jeshi la Polisi mkoa wa Mbeya kitengo cha Dawati la Jinsia na watoto limewataka wananchi kuwa chachu ya kukataa na kukemea matendo maovu ya unyanyasaji na ukatili katika jamii ikiwemo ulawiti kwa watoto..
Wito huo umetolewa na afisa wa jeshi la polisi Consolata Mng’ong’o ambaye ni afisa katika dawati la jinsia na watoto wakati akizungumza kwenye ibada ya sikukuu ya Wanaume wa katika kanisa la TAG Samaria Uyole jijini Mbeya.
Consolata amesema hivi karibuni kumekuwa kukishuhudiwa vitendo vya kikatili na unyanyasaji hivyo jamii inatakiwa kuwa ya kwanza kuchukia uovu huo na kushirikiana na Serikali ili kujenga kizazi imara cha sasa na baadaye.
Pia amekemea ukatili unaoendelea kufanywa na baadhi ya wanaume kwa kuwakataza wake zao kufanya kazi huku baadhi ya wanawake wakianzisha kiburi kwa wenza wao baada ya kuinuka kiuchumi mambo anayosema yanapelekea migogoro katika ndoa.
Naye Coplo Groly Mwanga kutoka Dawati la jinsia amewaasa wabinti kujiheshimu na kujitunza ili kufikia ndoto zao huku wakimtegemea Mungu wa kweli badala ya kujirahisisha kwa wanaume.
Mhubiri wa neno la Mungu Mwal. Boniface Jailo Ndeje amefundisha somo la wajibu wa mzazi kwa mtoto akiwataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawajali na kuwalinda watoto wao.
Kwa upande wake mchungaji wa kanisa la TAG Samaria Christian Centre Tazara Uyole Peter Masika ambaye ndiye askofu wa kanisa hilo Jimbo la Mbeya Kaskazini ameishukuru Serikali kwa kuendelea kusimama kidete kukataa mambo yanayokinzana na tamaduni za kiafrika na chukizo kwa Mungu.
Askofu Masika amewaasa waumini wake kuwa chachu kwa wenzao wakitumia elimu walioipata kuwalinda watoto wao na kukataa matendo ya unyanyasaji na ukatili miongoni mwao hasa waliookoka.
Makamu Mwenyekiti wa Idara ya Wanaume CMF Kanisa la TAG Samaria Adamu Mlawa amewashukuru maafisa wa Jeshi la Polisi hao kwa kushiriki ibada hiyo anayosema itakuwa chachu kijamii na kiroho na kuwashukuru wanaume wa Kanisa hilo kwa kufanikisha sikukuu yao ambayo imefanyika kitaifa katika TAG.