Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Wilbrod Mutafungwa akiwa ameambatana na wataalam mbalimbali wakiwemo kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Afisa Ustawi wilaya ya Magu, wamefika katika kijiji cha Salong’we, kata ya Mwamabanza, Wilaya ya Magu na kulazimika kufukua kaburi ambalo alizikwa mtoto aitwaye Mabilika Wilson aliyefariki Aprili 16 na kuzikwa Aprili 17 mwaka huu.
Aidha, tarehe 27.04.2023 muda wa saa 18:00 jioni Katika Kijiji cha Mwangika, Kata ya Mwabomba, Tarafa ya Ngulla ,Wilaya ya Kwimba, kuliripotiwa tukio la kuonekana kwa Mtoto aitwaye Mabirika Wilson, Miaka 8, Mkazi wa Kijiji cha Salong’we, Kata ya Mwamabanza, Wilaya ya Magu, baada ya vijana waliokuwa wanachunga Ng’ombe maeneo hayo kumuona mtoto huyo akiwa peke yake.
Taarifa hizo zilifanyiwa kazi kwa haraka ambapo Askari Polisi waliweza kumpata Baba Mzazi wa mtoto huyo aitwaye Wilson Bulabo ,Miaka 35, Pamoja na Mama wa Mtoto Aitwaye Helena Robert, Miaka 33, wote Wakulima na Wakazi wa Salong’we -Magu Ambapo waliweza kumtambua kuwa ni mtoto wao ambaye alifariki tarehe 16.04.2023 muda wa Saa 12:00 mchana kwa maradhi na Kuzikwa tarehe 17.04.2023 muda wa Saa 14:00 mchana huko Kijiji cha Salong’we, Kata ya Mwamabanza ,Tarafa na Wilaya ya Magu.
Baada ya mkanganyiko huo, Jeshi la Polisi kwa kuhusisha wataalam mbalimbali lililazimika kufukua kaburi ambalo alizikwa Mabilika Wilson ili kuweza kujiridhisha kama kulikuwa na mabaki ya Mwili wa mtoto huyo, baada ya kufukua mwili huo Wazazi walisema kuwa ule mwili sio wa mtoto wao bali wanamtambua yule aliyeokotwa Wilaya ya kwimba kuwa ndiye wao.
Ule usemi usemao “Ukistaajabu ya Mussa, utayaona ya filauni” umedhihirika pale mwili wa jinsia ya kiume unaokadiriwa kuwa na miaka 8 hadi 10 uliokuwa umezikwa mbele ya Nyumba ya Wilson ukikataliwa kuwa sio mtoto wao Mabilika Wilson waliomzika siku ya 17.04.2023 kijijini hapo.
Hivyo, mwili huo umechukuliwa kwa ajili ya uchunguzi kujua chanzo cha kifo chake pia kuchunguza yule mtoto aliyeokotwa kisha kutambuliwa na wazazi wao kuwa ni mtoto wao na kutambua jambo lililojifucha nyuma ya kifo cha mtoto huyo.