Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Mikataba ya ujenzi wa barabara saba (07) ambazo zimekuwa zikiongelewa kwa muda mrefu katika majukwaa mbalimbali ikiwemo ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakwenda kusainiwa hapo kesho Juni 16, 2023 tukio ambalo litashuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan
Hafla ya utiaji saini wa mikataba hiyo itafanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete mjini Dodoma ambapo barabara zote hizo zitajengwa kwa kiwango cha lami kupitia utaratibu wa EPC+ F (wa ujenzi wa manunuzi ya uhandisi pamoja na fedha).
Moja ya mkataba ambao utakwenda kusainiwa hapo kesho ni pamoja na mkataba wa ujenzi wa barabara ya kutoka Mafinga hadi Mgololo yenye urefu wa kilometa 81 ambayo itakwenda kujengwa kwa lami.
Hayo yamesemwa leo Juni 15, 2023 na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya akijibu swali la mbunge wa jimbo la Mufindi Kusini Mheshimiwa David Kihenzile aliyetaka kujua ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa.
Aidha, Mheshimiwa Kihenzile ameishukuru serikali ya awamu sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kukubali barabara hizo kujengwa kwa kupitia utaratibu wa EPC+F ambapo amesema italeta manufaa makubwa ya kiuchumi na kijamii katika jimbo la Mufindi Kusini na majimbo jirani barabara hiyo inapopita.
Miradi ya ujenzi wa barabara hizo ikikamilika itachochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi ambao barabara hizo zinapita pamoja na kurahisisha shughuli za usafiri na usafirishaji.