Na Frankius Cleophace Mara
Mahakama ya wilaya ya Tarime mkoani Mara imesema kuwa itaendelea kutoa kupaumbele kesi zinazohusu masuala la ukatili pamoja na kesi za watoto ili zisichukue muda mrefu katika utoaji maamuzi yake.
Hayo yamebainishwa na Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya yaTarime Vincencia Balyaruha kwenye mkutano wa mwaka wa wadau wa haki za ulinzi wa mtoto wilayani Tarime kilichoandaliwa na Jukwaa la Utu wa Mtoto CDF Tarime.
Hakimu Balyaruha amesema kuwa, kwa sasa mahakama ya watoto inakaa kila Alhamisi pia mara nyingi kesi zinazohusu watoto zikiwemo za ukatili zinapewa kipaumbele ili ziweze kusikilizwa na kumalizika mapema.
“Tumekuwa tukikutana mara kwa mara ili kuweza kuweka mikakati ya kumaliza kesi hizi mapema licha ya changamoto ya ushahidi lakini bado hatujakata tamaa” alisema Hakimu.
Pia Hakimu ameongeza kuwa suala la kumaliza kesi kiundugu bado linawapa changamoto kwani wahanga wa ukatili wamekuwa wakikwepa kutoa ushahidi na wakati mwingine kuacha kuhudhuria mahakamani, sisi kwetu ni changamoto kubwa.
Pia amesisitiza sana jamii kuendelea kuimarisha ulinzi kwa watoto ili kupunguza vitendo vya ukatili kwenye jamii mfano watoto wadogo chini ya miaka 08 pia na watoto wengine lazima walindwe.
Koshuma Mtengeti ambaye ni mkurugenzi wa Asasi ya Jukwaa la Utu wa Mtoto CDF amesisitiza jamii kuendelea kulinda watoto juu ya ukatili nakuwapa haki zao za msingi mfano kupatiwa elimu, mavazi pamoja na muda wa kuchezo jambo hilo litazidi kuwajengea uwezo mkubwa.
“Vyombo vya habari mna nafasi kubwa kwenye jamii hebu endeleeni kutoa elimu ikiwemo elimu ya ulinzi na usalama kwa watoto ili kupunguza ukatili ambao umekuwa ukitokea kwenye jamii zetu.” alisema Koshuma.
Naye kaimu mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Tarime Sylivanus Gwiboha amesema kuwa, serikali inaendelea kijipanga na kuweka mazingira rafiki kwa wahanga wa ukatili wa kijinsia ili waendelee kupata msaada kwa wakati..
Aidha, Mkuu wa wilaya ya Tarime Kanali Michael Mntenjele wakati akifunga kiako hicho cha mwaka amesema kuwa, sasa mashirika yote wilayani Tarime yashirikiane kwa pamoja ili kutoa elimu juu ya madhara ya ukatili wa kijinsia.