Na Joel Maduka, Geita..
Kufuatia changamoto ya uhaba wa vitanda vya kujifungulia kwenye Vituo vya afya vya Nyankumbu na Kasamwa Halmashauri ya mji wa Geita Mkoani Geita huku Zaidi ya watoto 500 wamekuwa wakizaliwa kwenye vituo hivyo.
Kufuatia Changamoto hiyo imeulazimu umoja wa wafanyakazi wanawake wa Mgodi wa Geita Gold Mining Limited (GGML) kutoa msaada wa vitanda vinne vya kisasa katika vituo hivyo vyenye thamani ya shilingi milioni (24) kwa ajili ya kulinda usalama wa mama na mtoto wakati wa kujifungua.
Akizungumza wakati wa kukabidhi vitanda vinne Mwenyekiti wa Wanawake wanaofanya kazi mgodini wa GGML, Lina Sitta amesema wameguswa kutoa msaada wa vitanda vya kujifungulia kutokana na namna ambavyo wameona mazingira yasiyo rafiki kwa Wanawake.
Hata hivyo kwa upande wake Meneja Mwandamizi anayeshughulikia masuala ya mahusiano ya mgodi wa GGML, Gilbert Mworia ameongezea kuwa wao kama mgodi wataendelea kusapoti shughuli za maendeleo ikiwemo miundombinu ya afya kwa lengo la kuboresha mazingira yaliyosalama kwenye Sekta ya afya ambayo yatawasaidia kuona jamii inayowazunguka inanufaika na uwepo wao.
Aidha Mkuu wa Wilaya ya Geita, Cornel Magembe amepongeza hatua ya mgodi huo kwa namna ambavyo umeguswa na kutoa msaada wa vitanda ambavyo vitasaidia wanawake kujifungua salama.