Home KITAIFA DKT. MAGEMBE AWATAKA WATUMISHI WA AFYA KUZINGATIA UADILIFU

DKT. MAGEMBE AWATAKA WATUMISHI WA AFYA KUZINGATIA UADILIFU

NA ENEA MWANJA, MBOZI SONGWE.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt Grace Magembe, amewataka watumishi wa Afya katika Mkoa wa Songwe kufanya kazi kwa kuzingatia maadili huku akiwapongeza watumishi hao mkoani humo kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya.

Dkt. Magembe amesema hayo wakati wa ziara ya kutembelea Kituo cha Afya cha Isansa, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe na Hospitali ya Wilaya ya Mbozi Mjini Vwawa.

Amesema “Sisi wateja wetu ni wananchi wanakuja kupata huduma. Wahudumiwe kwa wakati wapate huduma bora, kama mpo bize wapeni taarifa wagonjwa na ndugu wanaosubiri”.

Pia Dkt. Magembe amesisitiza kufanyika ukaguzi wa mara kwa mara wa dawa, vifaa tiba na huduma zinazotolewa.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia anatoa pesa nyingi katika sekta ya afya, ukaguzi unasaidia kuwa na kumbukumbu halisi maana mali bila daftari huisha bila habari”, amesisitiza Dkt. Magembe.

Vilevile amewataka viongozi wa vituo vya afya na hospitali kufanya vikao na watumishi ili kujua mahitaji yao.

Pia, amewataka watumishi kuwa na lugha nzuri akisema kuwa lugha nzuri ni dawa kwa mgonjwa anapofika hospitalini.

“Lugha nzuri ni dawa hata kama hujampa dawa mgonwa ukimpa maneno mazuri anafarijika”, ameeleza Kiongozi huyo na kuongeza.

“Tukiwajibu vibaya tutasemwa vibaya tusichoke haya ndio majukumu yetu tufanye kazi kwa weledi”, ameeleza.

Dkt. Magembe ambaye aliambatana na Naibu Katibu Mkuu wa Tamisemi (Afya) Dkt Charles Mahela amewataka watumishi hao kuepuka masuala ya rushwa.

“Suala la rushwa tuepukane nalo, tusimbague mtu kwa hali yake ukipatikana na rushwa ikathibitishwa Wizara ya Afya tutafuta usajili wako hutapata kazi ndani au nje ya nchi”, amebainisha.

“Msifanye kazi kwa mazoea kuna utaratibu wa kazi ufuatwe, kama watumishi wa afya tunawajibu wa kuhakikisha afya za wananchi zinalindwa”, ameeleza

Amewapongeza Kituo cha Afya cha Isansa kwa kuwa na chumba maalumu cha watoto wachanga ambao wanazaliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo upungufu wa uzito.

“Niwapongeze kwa kile chumba cha watoto wachanga zamani huduma hizo zilikwa zinapatikana katika level ya wilaya lakini Isansa kiipo”, amesema.

Ametoa rai kwa wananchi wa Kata ya Isansa kuwapa ushirikiano watumishi wa kituo hicho ili waweze kuwatumikia kwa muda mrefu na kutoa huduma bora.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Tamisemi (Afya), Dkt Charles Mahela amewamepongeza watumishi wa afya katika mkoa huo kwa kazi nzuri na kusema kuwa Serikari imewekeza sana katika sekta ya afya.

“Tamisemi kazi yetu ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora. Mheshimiwa Rais amewekeza sana katika huduma za afya” amesema.

“Ma-medical officers hakikisheni mnafuata miongozo ya Serikali sisi kazi yetu ni kuboresha maslahi yenu na kuwaongezea watumishi” ameelekeza Dkt. Mahela.

Previous articleJK NA MKEWE WATEMBELEA JAMII YA WAHADZABE
Next articleWASIMAMINZI WA NDOA NA VIONGOZI WA DINI WATAKIWA KUTOA ELIMU YA MALEZI KWA WANANDOA

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here