Msemaji mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu Charles Hillary amewataka waandishi wa habari kuwa na mazoea ya kujifunza kila mara ili kuweza kunoa na kukuza umahiri wao katika utoaji wa habari.
Hillary ameyasema hayo katika maadhimisho ya miaka 30 ya uhuru wa vyombo vya habari yaliyofanyika kitaifa Zanzibar ambapo amesisitiza ukuaji wa vyombo vingi vya habari usiwe ni kigezo cha uendeshaji holela usiofuata maadili ya taaluma hiyo.
Charles Hillary ambaye ni nguli katika habari kwa miaka 43 sasa amesisitiza suala la kujifunza na kufuatilia mambo mbalimbali yanayoendelea ulimwenguni ikiwa ni pamoja na kuibua changamoto zinazoikabili jamii.
“Miaka 30 imenikuta mimi nipo kwenye tasnia ya habari kwasababu sasa hivi nina miaka 43 na bado nipo kwenye tasnia ya habari lakini hainifanyi nisijifunze kwani kila siku mambo mapya yanaibuka”
Akizungumzia kuhusu baadhi waandishi wa habari kufanya kazi kwa kutofuata maadili na tofauti iliyopo kwa sasa kuwa ni kuongezeka kwa waandishi wa habari ambao wengi wao hawajapitia mafunzo ya uandishi wa habari “Mtu akijiona anasauti nzuri au anaweza akapiga picha na kuandika anajiita mwandishi lakini uandishi hauko hivyo inabidi wasome na waelekezwe pia” amesema
Akitolea mfano wake amesema imetokana na kufuata maelekezo ya wasimamizi wake katika tasnia na kuwa shida iliyopo kwa sasa ni vijana kujiona tayari wameshafika na wanaelewa na kupuuza ushauri wa kitaaluma unaotolewa na wazoefu.