NA JOSEA SINKALA, MBEYA .
Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Mkoa wa Mbeya Joseph Mwasote (China) amesema mkataba wa Bandari ambao Serikali imeingia na Dubai hauna manufaa kwa Taifa hivyo unapaswa kusitishwa mara moja kwa manufaa ya wananchi.
Mwasote almaarufu China wa China akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali wa CHADEMA akiwemo Katibu wa CHADEMA mkoa wa Mbeya Hamadi Mbeyale, John Mwambigija na Joseph Mbilinyi (Sugu) akizungumza katika eneo la KK Wilayani Rungwe amewataka wananchi hasa vijana kutokubali kuchaguliwa viongozi wasio wataka.
Pamoja na kuwataka wananchi kujiandaa na uchaguzi wa Serikali za mitaa na vijiji mwakani kwa kuchagua viongozi bora kiongozi huyo amenukuliwa akiukosoa vikali mkataba wa Bandari ambao unaelezwa kutokuwa rafiki kwa Tanzania.
Kwa upande wake aliyekuwa Mbunge wa Mbeya mjini Joseph Mbilinyi (Sugu) amesema Serikali imeshindwa kuongoza nchi kutokana na kukosa dira ya maendeleo endelevu huku akisema endapo Chadema itashika madaraka katika uchaguzi ujao itahakikisha inalinda mali za umma na kuhusu mkataba wa bandari ameitaka Serikali kutowalazimisha wananchi kuukubali.
John Mwambigija (mzee wa upako) aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mbeya mjini pamoja na kuzungumzia suala la bandari ambalo haliungi mkono kwa mkataba wake, amesema amejipanga kwenda kukomboa jimbo la Rungwe mwaka 2025 akidai uchaguzi wa mwaka 2015 aliibiwa kura.
Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Rungwe Seleman amesema kinga iliyowekwa na Serikali kwa baadhi ya viongozi kutoshtakiwa wanapokosea ni jambo lisilovumilika kwakuwa linafuga uhalifu Serikalini.
CHADEMA Kata ya Kyimo (KK) Tukuyu Wilayani Rungwe kimefungua mikutano hiyo ya hadhara ambayi itafanyika katika vijiji vyote vitano vya Kata hiyo ili kueleza itikadi na sera zake kuelekea chaguzi za serikali za mitaa na Uchaguzi mkuu wa 2025 ambapo agenda mama kwenye mkutano huo zilikuwa ni kueleza hali ya maisha ya wananchi ambayo gharama inaelezwa kuendelea kupaa kila uchao pamoja na kupingwa kwa mkataba wa kimataifa wa bandari ambao Serikali ya Tanzania imeingia kati yake na Serikali ya ufalme wa Dubai.