NA JOSEA SINKALA, MBEYA.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya imemhukumu kifungo cha Maisha jela mtu mmoja aitwaye Sadick Thomas baada ya kupatikana na hatia ya unajisi wa mtoto wa miaka sita.
Mahakama hiyo imetoa hukumu hiyo baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote mbili jamhuri na utetezi ambapo mshtakiwa Sadick Thomas A.K.A Baba Sasha baba Angel (46) mkulima na mkazi wa mkoani Mbeya anadaiwa kutenda kosa hilo mwaka jana.
Akitoa hukumu hiyo Hakimu Mkazi Sangiwa Mtengeti amesema mahakama yake imeridhishwa na ushahidi uliotolewa na jamuhuri kupitia mashahidi wake kadhaa akiwemo daktari aliyethibitisha mhanga kuingiliwa kimwili na mtu mzima.
Hakimu Mtengeti amesema ushahidi wa upande wa mashtaka haujaacha shaka yoyote mshtakiwa kutenda kosa hilo na kwamba ushahidi wa upande wa utetezi haujatia shaka kwenye ushahidi wa jamuhuri kwamba mshtakiwa alitekeleza uhalifu huo dhidi ya mtoto (6).
Hata hivyo kwenye utetezi wake mshtakiwa Sadick alikana kosa hilo kama ambavyo alikuwa akikana tangu afikishwe mahakamani licha ya Polisi kudai alikiri wakati akihojiwa baada ya kukamatwa lakini mshtakiwa huyo ameendelea kukana na kuiomba mahakama imwachie huru.
Wakati mshtakiwa Sadick akieleza azima yake kutombaka mtoto huyo, Mwendesha mashtaka wa Serikali Xaveria Makombe kwenye kesi hiyo namba 79/2022 ameiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshtakiwa ili iwe fundisho kwake na jamii kwa ujumla kutokana na kukithiri kwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji ikiwemo ubakaji na ulawiti kwa watoto.
Baada ya hayo Hakimu Mkazi katika mahakama ya hakimu mkazi Mbeya Sangiwa Mtengeti amemhukumu Sadick Thomas kwenda kutumikia kifungo cha maisha jela baada ya mahakama yake kuridhika na ushahidi kwamba alimbaka mtoto wa miaka sita ambaye ni mtoto wa jirani yake.