NA DENIS SINKONDE, SONGWE
MKUU wa wilaya ya Ileje mkoani Songwe Mhe. Farida Mgomi amesema jamii inapaswa kushirikiana katika kuwasaidia watoto yatima ili waweze kuishi kwa furaha kama walivyo watoto wengine.
Mhe. Mgomi ametoa kauli hiyo Julai 27,2023 katika siku ya watoto yatima iliyoandaliwa na kituo cha kulelea watoto yatima cha Isoko (ISOKO HOSPITAL OPHANS PROJECT) kilichopo Isoko kata ya Kafule wilayani humo.
Mhe. Mgomi amesema, suala la kuwasaidia watoto hao sio la hiyari, bali ni jambo lililoamrishwa na Mwenyezi Mungu lifanywe kwa kutegemea malipo mema kutoka kwake siku ya kiyama.
Aidha Mhe. Mgomi amefahamisha kuwa serikali itaendelea kuitekeleza azma hiyo kwa kuendelea kuwa nao bega kwa bega ili kung’amua kero na changamoto zao na hatimaye kuzitatua kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuwapatia malezi mema na waweze kuzifikia ndoto zao.
“Mmoja kufikiria kuanzisha vituo vya kusaidia watoto yatima au kupeleka misaada katika nyumba za kulelea watoto hao, pamoja na kuwa na utaratibu wa kuwatambua watoto yatima ambao hawaishi kwenye vijiji maalum, ili waweze kusaidia katika mahitaji yao muhimu anapaswa kupongezwa,” amesema Mhe.Mgomi.
Aidha Mhe.Mgomi ameyataja mahitaji hayo kuwa ni pamoja na elimu, kwani kuwapa watoto elimu ni sawa na kuisaidia nchi, kuinua vipaji vya watoto kielimu na kujenga mustakabali mwema wa hapo baadaye.
Mkurugenzi wa Kitengo cha kituo hicho, Enea Asangalwisye Kajange amesema Kitengo cha watoto yatima kinahudumia watoto 278 wakike wakiwa 160 na wakiume 118 ambao wanalelewa na kituo hicho Kwa kuwapatia mahitaji ya elimu ,malezi ya kimahitaji kama watoto wengine.